Chuo cha Ustawi wa Jamii

SIKU YA MTOTO WA AFRIKA DUNIANI JUNI 16,2024

Kwa kutambua umuhimu na changamoto wanazopitia watoto kote duniani, Afrika pamoja na Tanzania, hasa za kunyanyaswa kingono, kutumikishwa, kupigwa na kuuwawa, kusafirishwa, kubaguliwa na kutengwa hasa watoto wenye mahitaji maalum, #chuochaustawiwajamii kimeanzisha kozi ya malezi, makuzi na maendeleo ya awali ya mtoto ambayo inatolewa kwa ngazi ya cheti mpaka stashahada kwa lengo la kutatua changamoto za watoto wa kitanzania za ukosefu wa wataalam wenye ujuzi wa kuwasaidia watoto wanapokuwa au wanapopatwa na shida katika vituo vya kulelea watoto mchana, hospitali, masokoni, mitaani na sehemu nyingine katika jamii yetu ila kuhakiisha mtoto anakuwa katika utimilifu wake( kimwili, kiakili, kijamii na kimaono). #chuochaustawiwajamii Kitaendelea Kuwa mdau katika kuhakikisha Ustawi wa mtoto wa Kitanzania na kiafrikaa

WANAFUNZI CHUO CHA USTAWI WA JAMII KUIWAKILISHA TANZANIA MASHINDANO YA UBUNIFU BIASHARA (HULT PRIZE SUMMIT)– LONDON, Agosti 2024.

Wanafunzi watatu wanaosoma katika chuo cha ustawi wa jamii (Institute of Social work) kampasi ya Dar es Salaam wameibuka washindi wa pili katika mashindano ya ubunifu ambao unatokana na wazo la kutatua changamoto katika jamii na kubuni suluhu yake ambapo wazo hilo pia ni wazo la biashara. Ushindi wa wanafunzi hawa umetolewa na jopo la majaji na watu mashuhuri katika Nyanja za biashara na siasa katika mawasilisho ya Mawazo bunifu ambayo ni fursa za kibiashara zilizowasilishwa na wanafuzi kutoka nchi mbali mbali sabini (70) Duniani jijini Nairobi Kenya tarehe 7 Juni 2024 chini ya shindano liitwalo Hult prize. Wazo bunifu la Wanafunzi hawa kutoka Chuo cha Ustawi wa Jamii limetokana na ripoti za tafiti zikionyesha athari kubwa ya kijamii inayotokea katika bara la Afrika na hasa Tanzania kuwa na taka ngumu na laini nyingi katika Bahari na fukwe za Bahari ambapo kumeoneaka sampuli za taka ngumu katika viumbe Bahari na kuathiri usalama wa ukuaji na mfumo wa ikolojia ya viumbe Bahari lakini pia walaji wa mwisho wa samaki hawa kuwa katika hatari kiafya. Tatizo hili la kijamii likawafikisha Hellena Silas, Maria Daudi na Method Dallu kuanzisha timu yao ya Arena Recycling na kuanzisha mradi wa kukusanya taka hizi na kwa kutumia teknolojia maalum kuanza kuzalisha matofali kutumia taka hizo na kuwa wazo bunifu la kibiashara lakin pia likitatua changamoto ya kijamii. Timu hii ya Arena Recycling baada ya kufuzu Kwenda hatua nyingine ya ushindani katika bunifu yao hii itawakutanisha na timu nyingine 14 ambazo zilipatikana kutoka mashindano mengine ya kikanda na kutafuta mshindi wa kwanza na wengine katika mkutano utakao fanyika jijini London mwezi agosti 2024. Mshinda wa kwanza katika shindano hili anatarajiwa kupata kitita cha dola za kimarekani Milioni 1 (1 million USD) sawa na (2,610,500,112.28) Shilingi za kitanzania Bilioni mbili na milioni miasita katika kuendeleza bunifu zao kuwa mradi mkubwa zaidi.

CHUO CHA USTAWI WA JAMII CHATOA ELIMU KITUO CHA SARM’s OCCUPATIONAL THERAPEUTIC AND REHABILITATION JIJINI DAR ES SALAAM

Wahadhiri kutoka Chuo cha Ustawi wa Jamii watembelea na kutoa Elimu juu ya huduma kwa wateja na wajibu katika maeneo ya kazi kwa wafanyakazi wa kituo cha SARM’s Occupational Therapeutic and Rehabilitation kilichopo Kijitonyama Jiji Dar es Salaam Akizungumza wakati wa utoaji wa Elimu hiyo Mhadhiri Msaidizi Alexander Mwemfula kutoka idara ya Mahusiani kazini amewaasa na kuwataka wafanyakazi wa Kituo cha “SARM’s Occupational Therapeutic and Rehabilitation” kuzingatia utoaji wa huduma bora kwa wateja wanaofika kwa ajili ya kupata Huduma katika kituo hicho kinachojihusisha na utoaji wa Malezi kwa watoto wenye ulemavu. Kwa upande wao Mhadhiri Msaidizi Abdal Khamis Ali na Msaidizi wa Mhadhiri Nuru Pajenga wamewataka Wafanyakazi wa kituo cha “SARM’s Occupational Therapeutic and Rehabilitation” kuzingatia wajibu wao wawapo katika maeneo ya kazi na kuhakikisha hawaweki mbele maslahi yao binafsi na kusahau wajibu wao kulingana na makubaliano yao na Waajiri. Pia wamewataka wafanyakazi hao kuweza kudumisha nidhamu wawapo kazini kwani hiyo imekuwa ni moja ya sababu kubwa inayofanya watu wengi kupoteza ajira zao. Wafanyakazi hao pia walipewa fursa ya kuchangia mada na kuuliza maswali juu ya mambo yaliyo wasilishwa na wahadhiri wa Chuo cha Ustawi wa Jamii na wamekitaka Chuo kuendelea kutoa Elimu juu ya mambo mbalimbali yanayohusu mahusiano bora baina ya Wafanyakazi na Waajiri.

Wanafunzi Chuo cha Ustawi wa Jamii kushiriki Shindano la kimataifa Hult Prize Nairobi Kenya

Kupitia wazo Lao la kibishara na kibunifu linalohusu “Recycling of plastic waste into eco-brick “ (Utengenezaji na uzalishaji wa tofali kwa kutumia taka za plastiki) wanafunzi watatu kutoka #chuochaustawiwajamii ni Miongoni mwa wanafunzi kutoka vyuo mbali mbali Duniani wanaokutana Jijini Nairobi Nchini Kenya Kuwania Tuzo hii. Tuzo ya Hult ni shindano kubwa zaidi la ujasiriamali wa kijamii kwa wanafunzi duniani, Inayoendeshwa kwa ushirikiano na Umoja wa Mataifa na timu za wanafunzi kutoka vyuo vikuu mbalimbali duniani. Mashindano haya yanalenga kutatua tatizo la kijamii lenye umuhimu kwa kuanzisha biashara ya kijamii inayoweza kukua na kudumu. Washindi wa mwisho watawasilisha miradi yao mbele ya jopo la majaji mashuhuri, viongozi wa biashara duniani, viongozi wa mawazo, na watetezi wa mabadiliko ili kushinda dola milioni 1 za Marekani na kuanzisha biashara zao. Mkuu wa #chuochaustawiwajamii Dkt. Joyce Nyoni tarehe 04/06/2024 ameongea na wanafunzi hao ambao ni Hellena Sailas, Maria Daudi, na Method Dallu ambao tarehe 05/06/2024 waliwasili Jijini Nairobi tayari kwa Shindano hilo. Dkt. Joyce amewapongeza sana Wanafunzi hao wabunifu wa #ISW na kuwapa Mkono wa Kheri na kuwatakia Mafanikio katika Ushiriki wao.

WAFANYAKAZI BORA WATUNUKIWA VYETI

Wafanyakazi wa Chuo cha Ustawi wa Jamii wa muda mrefu, kutoka idara mbalimbali na wabunifu watunukiwa Vyeti. Hafla ya kuukaribisha Mwaka mpya na kufanya tathimini ya Mwaka 2023 ulimpa fursa Mkuu wa Taasisi kutunuku Vyeti kwa watumishi waliofanya kazi kwa muda mrefu, wabunifu pamoja na waliofanya vizuri katika idara na vitengo mbalimbali. Mkuu wa Chuo cha Ustawi wa Jamii Dr. Joyce Nyoni kabla ya ugawaji wa vyeti hivyo alimesema “Kila Mtu anamchango mkubwa katika ukuwaji na mafanikio ya Taasisi, hivyo tungetamani kila Mtu aweze kupata zawadi lakini tutawapatia wachache walionekana kufanya zaidi’’.

Wanawake Watumishi ISW Waigusa Jamii

Katika Matukio mawili tofauti Wanawake Watumishi wa Chuo cha Ustawi wa Jamii wametoa Zawadi na Elimu katika kuadhimisha Siku ya Wanawake Duniani. Wanawake Watumishi wa Chuo cha Ustawi wa Jamii Kampasi ya Kisangara, Mwanga Kilimanjaro wametembelea Shule ya Sekondari Nyerere na kutoa Elimu kwa Wanafunzi pamoja na zawadi mbalimbali ikiwa ni pamoja na Taulo za kike. Kwa Upande wa Kampasi ya Kijitonyama, Dar es Salaam Watumishi Wanawake wametembelea Shule ya Watoto wenye mahitaji Maalum ya "Sinza Maalumu" iliyopo Sinza jijini Dar es Salaam na kutoa zawadi na bidhaa mbalimbali za mahitaji muhimu. Matukio haya yamefanyika tarehe 05 na 06 Machi 2024.

ISW YAENDESHA MAFUNZO YA PROGRAMU WEZESHI KWA WANAFUNZI WENYE UONI HAFIFU

Chuo cha Ustawi wa Jamii kupitia ofisi ya mshauri wa wanafunzi kimefanikiwa kuandaa na kuendesha Mafunzo ya Programu wezeshi kwa wanafunzi wenye Changamoto ya uoni (wasioona). Program hii imefanyika mwishon mwa Mwezi Februari mwaka 2024 na imejumuisha jumla ya Wanafunzi nane wanaosoma katika Chuo cha Ustawi wa Jamii pamoja na wasaidizi wanne kwa ajili ya kuwaongoza Wanafunzi wenzao wasioona katika maeneo mbalimbali na kufanya programu hii kujumuisha Jumla ya washiriki kumi na mbili. Mafunzo haya ya Programu wenzeshi wameendeshwa chini ya Mkufunzi Honolath Ngowi kutoka katika Chuo Huria (Open University). Dhima kuu ya Mafunzo haya ni kuwawezasha Wanafunzi wasioona kuweza kuendana na mabadiliko ya Sayansi na Teknolojia yanayokuwa kwa kasi kila iitwapo leo. Katika mafunzo haya wanafunzi wamejifunza mambo mbalimbali ikiwa ni pamoja na ustadi katika matumizi sahihi ya kibodi wakati wa matumizi ya kompyuta.

Maendeleo ya Kasi Kampasi ya Kisangara

Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum Wakili Amon Mpanju amekipongeza Chuo cha Ustawi wa Jamii kwa Maendeleo ya kasi yanayoendelea katika Kampasi ya Kisangara. Wakili Amon Mpanju ametoa pongezi hizo wakati wa Mahafali ya 6 ya Chuo cha Ustawi wa Jamii Kampasi ya Kisangara, Mwanga Kilimanjaro Januari 26, 2024. ambapo jumla ya wahitimu 237 wametunukiwa tuzo mbalimbali. "Naipongeza pia Menejimenti ya Chuo kwa kusimamia vizuri ujenzi wa Hostel mbili zenye ukubwa wa kubeba wanafunzi 208, ujenzi wa mgahawa kwa matumizi ya wanafunzi na jamii nzima inayozunguka chuo. Nawapongeza pia kwa juhudi ambazo mmezichukua za kuhakikisha maji yanapatikana katika eneo letu la Chuo. Hakika hii itaifanya Kisangara iendelee kuwa ya kijani zaidi." Amesema Mpanju. Mpanju pia amefurahishwa na kuanzishwa kwa kozi ya Malezi, Makuzi na Maendeleo ya Awali ya Mtoto kwa ngazi ya cheti na diploma ambayo inatambuliwa na Baraza la Taifa la Elimu ya Ufundi na Mafunzo ya Ufundi Stadi (NACTVET), kuanzishwa kwa programu ya Shahada ya Ustawi wa jamii (Bachelor Degree in Social Work) inayotambuliwa na Tume ya Vyuo vikuu Tanzania (TCU) katika mwaka wa masomo 2023/2024 Kwa Upande wake Mkuu wa Wilaya ya Mwanga Mhe. Abdalah Mwaipaya akizungumza katika mahafali hayo amesema uwepo wa chuo cha Ustawi wa Jamii Kisangara ni muhimu kwa wilaya ya mwanga kwa kuvutia zaidi uwekezaji. Amewaasa wanafunzi kurudi Mwanga Kuendelei kusoma Chuo cha Ustawi wa Jamii Kampasi ya Kisangara. Naye Naibu Kamisha wa Ustawi wa Jamii Tullo Masanja amewakumbusha wahitimu kuwa ndiyo madaktari wa jamii kutokana na ongezeko la tatizo la afya ya akili, hivyo wanatakiwa kutumia utaalamu waliopata kuhakikisha wanalinda na kuokoa jamii, hasa mmomonyoko wa maadili. Dkt. Lulu Mahai (Kaimu Mwenyekiti wa Bodi ya Magavana ya Chuo) Ameeleza Jinsi ambavyo kampasi inakabiliwa na changamoto ya jengo la utawala na ufinyu wa jengo la maktaba ukizingatia ongezeko la wanafunzi baada ya kuongeza Programu mbili za Kitaaluma katika kampasi hiyo.

KONGAMANO LA 10 LA KITAALUMA LAJADILI ujenzi wa ujuzi na ushirikishwaji wa watu wenye wenye mahitaji maalum katika shughuli za maendeleo

Wadau, wanataaluma na wanafunzi wameshiriki katika kongamano la 10 la kitaaluma (Convocation) juu ya ujenzi wa ujuzi na ushirikishwaji wa watu wenye wenye mahitaji maalum katika shughuli za maendeleo. Akizungumza leo Desemba 7, 2023 jijini Dar es Salaam wakati akifungua kongamano hilo , Naibu Mkuu wa Chuo Prof.Sotco Komba Taaluma amesema chuo kimejikita zaidi katika maboresho ya watu wenye ulemavu ili kukuza ujuzi katika nyanja ya maendeleo ya kiuchumi ili waweze kushirikia michakato mbalimbali ya maendeleo katika taifa letu. Dkt. Nassib Mwaifunga, mtaalam wa masuala ya Uchumi na Fedha na Sheria kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu amewataka vijana kuchangamkia fursa mbalimbali kutoka ofisi ya Waziri Mkuu hasa walemavu ili waweze kujikomboa kiuchumi na kukuza maeneleo katika maisha yao ya kila siku. Aidha aliwataka vijana ambao ni wanafunzi kwenda na wakati katika mafunzo na masomo wanayochukua ili waweze kwenda na kasi ya soko la ajira duniani. Amebainisha fursa kubwa hasa ajira ambazo zinapewa kipaumbele kwa kuzingatia ujuzi iko katika kiwango kikubwa katika kozi za mafuta na gesi, usafirishaji, afya na vifaa tiba na madini. Mbali na hilo amewataka waajiri nchini kuachana na dhana ya kudharau watu wenye mahitaji maalum hasa katika kuwapa ajira kwani watu hao wana uwezo mkubwa wanapopewa nafasi. #chuochaustawiwajamii kimepongezwa kwa kuanzisha kitengo maalum utoaji wa huduma kwa wanafunzi wenye mahitaji maalum na ni mfano wa kuigwa na vyuo vingine nchini Umekuwa ni utamaduni wa Chuo cha Ustawi wa Jamii kufanya kongamano hili la kitaaluma kila mwaka kabla ya mahafali yake, ambapo kwa mwaka 2023 mahafali hayo yatafanyika tarehe 08/12/2023 katika ukumbi wa JKT mwenge.

ISW Yashinda Tuzo Uandaaji Taarifa za Hesabu za mwaka 2022

Mkuu wa Chuo cha Ustawi wa Jamii Dkt. Joyce nyoni akiwa pamoja na baadhi ya wahasibu wa #ISW akipokea tuzo ya mshindi wa tatu ya uandaaji wa taarifa za hesabu chini ya viwango vya IPSASs 2022, katika kundi la vyuo vya elimu ya juu nchini kwa mara nyingine. Tuzo hiyo imetolewa jioni ya tarehe 1, Disemba 2023 na NBAA katika hafla maalum ya kutoa tuzo hizo.

BONANZA LA MICHEZO KUELEKEA KILELE CHA MIAKA 50 LAZINDULIWA

Dkt. Happy Mwakajila kwa Niaba ya Mkuu wa Chuo cha Ustawi wa Jamii Dkt. Joyce Nyoni amefungua Bonanza la Michezo ikiwa ni sehemu ya shughuli mbali mbali kuelekea Kilele cha Miaka 50 ya Chuo ambapo timu ya Mpira wa Miguu ya Wanaume #ISW imepimana nguvu na timu ya watumishi wa Hospitali ya Ocean Road Dar es Salaam ambapo timu zote mbili zimetoka sare ya bila kufungana katika mechi hiyo. Michezo hiyo itakutanisha Taasisi na vyuo mbali mbali ikihusisha wanafunzi na watumishi katika michezo mbali mbali.

NAIBU KATIBU MKUU WAKILI AMON MPANJU AFANYA KIKAO KIFUPI ISW

Naibu Katibu Mkuu, Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum Wakili Amon Mpanju amefika katika Chuo cha Ustawi wa Jamii leo tarehe 10/11/2023 na kukutana na baadhi ya Wajumbe wa Menejimenti ya chuo ili kupata taarifa ya hali ya utoaji huduma, maendeleo ya miradi ya chuo na vile vile kutoa maelekezo na ushauri katika kuboresha utoaji huduma na utekelezaji wa miradi ya chuo.

CHUO CHA USTAWI WA JAMII CHAFANYA MAWASILISHO YA TAFITI ZA KITAALUMA.

Chuo cha Ustawi wa Jamii leo tarehe 10/11/2023 kimefanya mawasilisho ya tafiti mbili za kitaaluma ambazo imezifanya katika mada mbili tofauti ikilenga kutafuta kina cha suluhu ya matatizo ya hali mbali mbali yanayotokea katika jamii ya kitanzania. Akiwasilisha taarifa za tafiti hizo mmoja wa mtafiti kiongozi wa tafiti hizo Mhadhiri Mwandamizi Dkt. Zena Mabeyo amesema wamefanya tafiti mbili ambazo ni: - ‘’kuchunguza kanuni, maadili na mbinu zinazowalinda wanawake dhidi ya unyanyasaji Tanzania: uchunguzi kesi ya mikoa ya Mbeya, Mara na Tanga’’ na kuathirika kwa wafanyakazi wasio rasmi katika muktadha wa Uviko 19: kesi ya sekta ya utalii mkoani Kilimanjaro na Arusha. Kwa taarifa Zaidi tembelea ; https://www.isw.ac.tz/assets/doc/Dissemination_brief_PROWOMEN.pdf, https://www.isw.ac.tz/assets/doc/REPOA_FINAL_EDITED_POLICY_BRIEF_07_11_2023_(1).pdf

KARIBUNI - ISW

Mkuu wa Chuo cha Ustawi wa Jamii Dkt. Joyce Nyoni amefungua Mafunzo ya awali kwa watumishi wapya ISW. Akiongea katika ufunguzi wa mafunzo hayo katika kampasi ya Dar es Salaam, Dkt. Joyce amewapongeza watumishi hao wapya na kuwaasa kuwa waadilifu, wachapakazi, kufanya kazi kwa weledi, na kutoa huduma bora kwa wateja wa Chuo cha Ustawi wa Jamii.

Site Visitors
Today
539
Yesterday
1,305
This Week
11,395
This Month
41,024
All days
324,014
Online
3
Video